Thursday, October 28, 2010

http://wapichai.ning.com/profile/msafiriabdallah

MSAFIRIs VUVUZELA: HADITHI

MSAFIRIs VUVUZELA: HADITHI

VITUKO MITAANI

Kuna dada mmoja hajaolewa anakaa nyumba ya kupanga pamoja na wengine ambao wameolewa. Dada huyu alikuwa na tabia ya kila wakati kwenda kuoga akiwa amevaa taulo tu. Kitu hiki hakikuwapendeza wenzake ambao wameolewa kwa kumwona kama anawatega waume zao.




Siku moja wenzake wakapanga njama za kumkomesha. Wakamtafuta mtoto wa mitaani na kumuagiza amvizie anapokwenda kuoga amnyang'anye taulo akimbie nalo. Kwa bahati wakati wanapanga njama hizo dada mhusika alikuwa amejibanza kwenye chumba chake anawasikiliza.



Siku ikafika ya utekelezaji wa njama hizo. Yule dada kama kawaida yake na bila wasiwasi akavaa taulo lake bila kitu kingine kwa ndani na kuelekea kuoga kwenye bafu la nje.



Ghafla akiwa katikati ya nyumba na bafuni yule kijana akatokea na kupora taulo akakimbia nalo. Kipindi hicho karibia wapangaji wote walikuwa hawakucheza mbali wapo jirani jirani kushuhudia matokeo ya mpango wao.



Kinyume cha matarajio yao, yule dada baada ya kuporwa taulo hakustuka hata kidogo kana kwamba hakuna kilichotokea. Akaendelea na safari yake bafuni akiwa mtupu. Baada aya kumaliza kuoga, akatoka bafuni na kuelekea vyumbani kama alivyozaliwa.



Wapangaji wenzake ikabidi wapeleke mashtaka kwa mjumbe na yule dada akaitwa ajieleze kisa cha kuwamwagia radhi wenzake.



Alichosema yule dada, nanukuu "......nashukuru mjumbe kwa kunipa nafasi ya kuongea......kabla ya yote naomba nikukabidhi mchango wangu wa shs 20,000/= ili akaongezewe yule mtoto aliyepewa pesa na wapangaji wenzangu aje anipore taulo wakati ninakwenda kuoga........pili, sioni kwa nini tumeitana kwa sababu kila mtu anajua kuwa matokeo ya kuvuliwa nguo ni kubakizwa uchi, na mimi kwa kulijua hilo nikadhani pengine wenzengu wangependa kuniona nikiwa sina taulo......vinginevyo wasingelimkodi mtu aninyang'anye taulo akimbie nalo kwani wao walitarajia iweje......kwa ujumla mjumbe kama kunatafutwa mkosaji basi ni hawa wenzangu......na kama tunataka kutenda haki.....hawa ndio wanilipe mimi fidia kwa kunidhalilisha kwani taulo sikujivua mwenyewe"



Mjumbe akabaki mdomo wazi.

Tuesday, August 24, 2010

BI ZAINABU SHAHIDI - (sehemu ya kwanza)

BI ZAINABU SHAHIDI - (sehemu ya kwanza)




Nilikuwa najipitia tu asubuhi pale makutano ya mtaa wa Swahili na Mafia; saa moja asubuhi naelekea kazini mitaa ya Samora. Nilikuwa natoka Buguruni kwa mabasi yaendayo Muhimbili nikiwa nimeshukia kituo cha Msimbazi.





Siku hiyo niliamka na nguvu maana mfukoni nilikuwa na kama shilingi laki tatu hivi; ni mara chache kwangu kuamka hivyo na nina imani kwa watu wengi wa aina yangu katika jiji hili pia siyo kawaida hata kwao.



Katika makutano hayo upande wa kulia huwa kuna akina mama wengi sana wamejipanga mstari wameketi na vyombo vyao vya makulaji wakiuza kujitafutia riziki. Mahali hapa kila aina ya kitafunio kinachopatikana nchi hii uliweza kukipata, na pia kila aina ya supu isipokuwa moja tu ile ya Iringa; zote zilikuwa zikipatikana.



Siku hiyo mwenyewe nilishapita kona hiyo lakini kama vipi vile kitu kikaniambia ebu angalia nyuma....hapo ndipo nilipoona hicho nilichokiona.



Sijaelewa ni kwa nini jicho langu moja kwa moja lilifika kwake lakini hivyo ndivyo ilivyotokea.



Alikuwa ni Dada wa miaka kati ya ishirini na tano na therathini. Japo alikuwa ni dada wa kawaida lakini kwa kweli alikuwa mzuri. Kwangu mimi hilo la uzuri halikuwa sana lakini nadhani kuna kitu ambacho kilinigusa zaidi kuhusiana na huyo dada.



Pale mbele yake alipokaa palikuwa na sufuria saizi ya kati limefunikwa likiwa juu ya ndoo. mwenyewe alikuwa kajitanda au sijui kama ni kuvaa ushungi wa rangi ya zambarau na gauni la maua ya kijani na samawati. Nilisimama pale nilipokuwa nimefika na kuendelea kumtazama vizuri ili niweze kukiona kitu ambacho kilinifanya niendelee kumwangalia yeye na si mwingine kati ya kundi zima lililokuwepo mahali pale. Zilipita takribani dakika kumi nzima bila kuona chochote. Nilikuwa kama nimepigwa na bumbuazi hadi nilipokuja kugutuliwa na teja mmoja kwa kunikumbusha kuwa nilikuwa nimesimama barabarani na kwa kipindi ambacho nimesimama pale nilikuwa nimekoswakoswa kugongwa na magari matatu.



Pamoja na masaada wa teja, kilichoweza kinirudia ilikuwa ni fahamu lakini uamuzi wa kuondoka pale nilikuwa bado sijaufikia.



Idadi kubwa ya akina mama pale walikuwa hawajajua kinachoendelea, kama ujuavyo biashara ni asubuhi kila mmoja alikuwa na hamsini zake, hata yule bibie niliyekuwa namwangalia, kwa dakika tano za awali alikuwa hajajua kuwa namwangalia japo baadae aliniona na kubaki akinishangaa.



Sijui kama ni kwa kukerwa au kwa huruma, dada yule aliinuka pale alipokuwa na kunifuata niliposimama akaniuliza kama nilikuwa na mfananisha na mtu ama kulikoni. Kwa hapo sikuwa na jibu zaidi ya kumwuliza kama ulikuwepo uwezekano wa mimi na yeye kukutana mahali mbali na sehemu ile tuweze kuongea zaidi. Ilikuwa kama alikuwa anategemea nitasema vile; alinishauri tukutane Concord Hotel saa saba na nusu mchana na akasisitiza niende na muda kwani hatanisubiri zaidi ya robo saa. Sikusema chochote zaidi ya kuitikia kwa kichwa na kuondoka.



Wakati tayari nimekwisha fika ofisini, ndipo nilipokumbuka kuwa nimefanya makosa mengi sana ya kiufundi. Yule dada sikumwuliza jina na wala sikumwomba namba yake ya simu wala kumpa yangu; hiyo kitu sikuipenda japo nilijipa moyo kuwa makosa kama hayo ni ya kawaida kama ambavyo Ronaldo ama Drogba anavyoweza kukosa panati katika mechi muhimu.



Ikiwa imebaki nusu saa kufikia saa saba na nusu niende kukutana na dada niliitwa ofisini na bosi kutoa taarifa juu ya safari ambayo nilikuwa ninerejea siku mbili zilizopita. Nilijua pengine dakika kumi zingelitosha kuwasilisha taarifa ile kwa kuzingatia kuwa nilikuwa nimeiandika; lakini mambo yalikuwa sivyo hadi inafika saa saba na dakika ishirini bado bosi alikuwa anaendelea kuungurumisha maswali.



Kwa kuona sasa ipo hali ya hatari ya kuikosa ahadi nilimwomba bosi nikajisaidie kwani nilikuwa najisikia tumboni mambo si shwari; alipokubali tu nilichomoka kama chizi na kutokomea mtaani badala ya kwenda uani palepale ofisini. Niliamua nifanye vile kama kutakuwa na hoja basi ni hapo baadae ili mradi nimetimiza ahadi.



Kwa kuona muda ulikuwa umeyoyoma niliamua nichukua teksi inikimbize kwani toka mtaa wa Samora hadi ilipo hoteli ya Concord kulikuwa na umbali. Lakini kama wasemavyo wahenga kuwa ngombe wa maskini hazai na akizaa anazaa dume na dume lenyewe linakufa; hivyo ndivyo ilivyonitokea. Pamoja na jitihada zote za kutaka kuwahi, nilifika Concord Hotel saa nane kasoro dakika kumi. Sikusubiri gari lisimame kwani tayari tulikuwa tumekwisha lipana na dereva. Nilichomoka na kuingia fosi mapokezi kuulizia kama kuna mgeni yeyote yupo hapo anamsubiri mtu; dada wa mapokezi akanifahamisha kuwa alikuwepo dada mmoja ambaye alikuwa amekaa kwa karibu nusu saa hivi lakini muda si mrefu ameondoka kwa gari aina ya Range Rover.



Mwanzoni sikukubaliana na mtu wa mapokezi kuwa anayemsema ndiye niliyemfuata lakini baada ya kupata maelezo ya kina kuwa yule dada alipokuwa akiondoka pale alisema kwa kuwa mwanaume aliyekuwa ameahidiana wakutane pale saa saba na nusu alikuwa amechelewa basi yeye anaondoka. Ama kwa hakika baada ya kupata habari ile nguvu ziliniishia.





*******************

Saturday, August 14, 2010

TONE LA HUBA

TONE LA HUBA




Nilikuwa nimepanga mtaa wa Majani kwenye nyumba ya Mzee Mbinde; nyumba iliyokuwa na vyumba kumi na viwili vilivyojengwa kwa safu mbili zinazitazamana.



Chumba changu kilikuwa ni cha mwisho kulia ambacho mlango wake ulikuwa ukitazamana na mlango wa chumba cha Seme.



Seme alikuwa ni mvulana mwenye umbile la kadiri kwa kila namna; yaani mfupi kiasi mwembamba kiasi, mweupe kiasi ili mradi kwa ninavyovijua ilikuwa ni kiasi kiasi kiasi.



Mimi mtaa mzima walikuwa wamezoea kuniita Mammy lakini jina langu kamili ninaitwa Mamamia.



Katika nyumba hiyo ya Mzee Mbinde, mimi ndiye nilianza kupanga kabla ya Seme ambaye alihamia hapo baada ya miaka miwili.



Wapangaji wenzetu na majirani wengi hawakumpenda Seme kutokana na mambo yake hayo ya kiasi kiasi; wengi walimwona msiri, mwenye maringo na roho mbaya tofauti na mimi ambaye kwa hakika nilimwona kama kipande dha almasi katika chupa ya kioo isiyofunguka kirahisi.



Tangu ahamie pale nilikuwa nikijitahidi sana kutafuta fulsa ya kuongea nae lakini daima alikuwa na salamu za kiasi na majibu ya kiasi; kiasi kwamba kama si mapenzi ya dhati juu yake na mimi ningeliungana na majirani kumwona si chochote.



Kwa kweli Seme alikuwa ni mvulana wa aina yake. Sikupata kujua anakula saa ngapi, wapi na anakula nini. Sikuwahi kumfahamu rafiki yake, ndugu yake, kabila yake wala dini yake. Seme alikuwa ni ingia toka, sikuijua shughuli yake wala aendako na ashindako muda wote.



Kwa miaka yote nilikuwa ninasumbuka na ninataabika kwa subira kwa imani kuwa ipo siku milango ya Seme itafunguka ili niweze kuupenyeza moyo wangu lakini kinyume na matarajio kila siku iliyokuja ilikuwa ni aheri ya siku iliyopita. Moyo wangu ulizidi kujazwa kutu ana mwenendo wa mwanaume huyu.



Kunako siku ya siku mimi sikulala nilikesha nikiwaza. Hivi ni kwa nini nipate shida hii na huyu anayenipa matatizo yote haya ni nani hasa; ndipo siku hiyo nikapitisha maamuzi kuwa haiwezekani, lazima nimjue huyu Seme kwa undani na baada ya hapo ni nipitishe azimio la mwisho.



Siku hiyo niliamka mapema, nikaoga na kuvaa suruali nzito nyeusi na fulana nyeusi tayari kwa kazi ya ukachero ambayo sikuijua itaishaje. Kwa hofu ya kazi hiyo nikachukua kiasi cha shilingi laki nane ambazo nilikuwa ninazihifadhi nyumbani nikazitia katika mkoba wangu mdogo mweusi. Kwa tahadhari zaidi, nikachukua kitambulisho changu cha kazi, pasi ya kusafiria na kitambulisho cha mpiga kura.



Wakati nakamilisha kufanya vyote hivyo nikasikia mlango wa Seme ukifunguliwa nikajua sasa kazi inaanza.



Nilimwacha kwanza Seme atangulie kidogo, ndipo nilipofunga mlango wa chumba changu na kuanza kumfuata Seme. Seme bila ya wasiwasi wowote alitembea bila ya kugeuka nyuma, na mimi nikawa namfuata bila ya kugeuka nyuma kwa kuhofia kuwa ninaweza wakati mimi nimegeuka, Seme nae akageuka na kuniona bila mimi kujua.



Seme alikata mitaa miwili, kisha akaenda panapo teksi moja ya kukodi. Hapo sasa jasho lilianza kunitoka, lakini nikasema sikubali ni mimi na yeye leo.



Wakati teksi yake inaondoka na mimi tayari nilikuwa katika teksi namwelekeza dereva aifuate teksi iliyokuwa ikiondoka mbele yetu.



Safari ya kufukuzana na Seme ilianza kwa kutumia magari ambayo si yetu na hatukuwa na mamlaka nayo.



Teksi ya Seme ilikuwa ikiendeshwa kasi kuelekea nje ya jiji. Dareva wangu nae alikuwa akijitahidi sana kuifukuzia teksi hiyo lakini kwa tahadhari ya kutoonekana na kutopata ajali japo usoni nilimwona mwenye mashaka.



Nilimtia moyo aendeshe kwani fedha siyo tatizo.



Kwa mbele yetu akina Seme waliingia kituo cha mafuta na hapo nikamwona na dareva wangu akipumua kwa furaha, kumbe shaka yake ilikuwa ni kuishiwa mafuta wakati ukimfukuzia mtu. Tulipunguza mwendo na kuwaacha wajaze na sisi tujaze.



Baada ya shughuli hiyo kazi ya kufukuzana iliendelea.



Sikuamini macho yangu tukiwa katikati ya pori gari ya mbele yetu iliposimama na kumshusha Seme. Kwanza nilipigwa na butwaa kabla sijatoa maelekezo kwa dareva wa teksi niliyoikodi aegeshe gari kwa pembeni nishuke kisha afanya kama anapita akageuzia mbele aje asimame pale niliposhukia.



Nikimlipa pesa yake kwanza haraka haraka na kumwomba namba ya simu endapo nitamhitaji nitampigia.



Nilianza kunyatia kwa nyuma kufuata Seme. Seme alikuwa akiyoyoma ndani ya msitu kama hana akili nzuri. Kama kawaida yake alikuwa hatazami nyuma. Tuliupita msitu, tukaikuta mbuga baadae tukaanza kuiona bahari. Moyo ulianza kunidunda kwa kasi kwa hofu ya huko anakoelekea Seme; lakini kwa kuwa maji ukiyavulia nguo ni lazima uyakoge niliendelea na msafara hadi nikamwona Seme amesimama kando ya bahati.



Hapo aliposimama seme ndipo nilipoanza kuyaona maajabu, nikamwona Seme anainama na kufungua kitu kama mlango chini na kuanza kushuka kitu kama ngazi. Baada ya Seme kupotea na mimi nikaenda eneo hilo hilo, mwanzoni sikuuona mlango huo lakini baadae nikauona. Namimi nikainama na kuufungua, ni kweli nilikuta kuna ngazi zinashuka chini.



Bila ya kuwa na uhakika na ninalolifanya nilitelemka kwa kasi hadi katika chumba ambacho ama kwa hakika tangu nizaliwe sijapata kuona chumba kizuri kama kile. Kwa kuwa hakukuwa na kunakoendelea na Seme simwoni na wala sioni mlango mwingine zaidi ya nilioingilia nikaamua nikae kwenye viti vizuri vya chumba hicho nisubiri kiama changu.



Nilikaa kwa karibu nusu saa nzima lakini sikumwona Seme wala kusikia mlio wowote. Niliendelea kukaa vilevile hadi usingizi uliponipitia.



Nadhani nililala kwa muda mrefu sana hadi jioni nilipoamshwa na Seme lakini tofauti na ilivyokuwa niliamka nikiwa chumbani tena kitandani kwa Seme na Seme mwenyewe amesimama akiniangalia kwa mshangao..."..Mammy umeingiaje chumbani kwangu wakati ufunguo ninao mwenyewe !"



Mpaka hapo sikuwa naelewa kama yanayotokea ni kweli ama ninaota.